JK AONGOZA MAHAFALI YA 55 (DURU LA PILI) YA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM UKUMBI WA MLIMANI CITY JIJINI DAR

UDSM yamtunuku Dkt. Maria Kamm Shahada ya Heshima kutokana na mchango wake katika elimu nchini DAR ES SALAAM MKUU wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambaye ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ametunuku Shahada za Awali, Stashahada na Astashahada kwa wahitimu katika Mahafali ya 55 (Duru la Pili) ya chuo hicho kikongwe kuliko vyote nchini. Jumla ya wahitimu 2,742 walihudhurishwa kwenye mahafali hayo yaliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.
katika hatua nyingine Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimemtunuku Digrii ya Heshima ya Udaktari wa Fasihi Mwasisi na Mwenyekiti wa Taasisi ya Mama Clementina, Dkt. Maria Josephine Kamm, kutokana na mchango wake mkubwa na wa muda mrefu katika kuendeleza elimu nchini. Tuzo hiyo imetolewa leo, Novemba 18, 2025, wakati wa mahafali ya 55 ya UDSM yaliyofanyika katika ukumbi wa Mlimani City, yakihudhuriwa na maelfu ya wahitimu, wazazi na wageni waalikwa. Akizungumza baada ya kutunukiwa, Dkt. Kamm amesisitiza umuhimu wa kumwezesha mtoto wa kike kupata elimu bora, amesema hatua hiyo hubadilisha si maisha ya mtu mmoja pekee, bali pia jamii nzima na hata taifa kwa ujumla.
“Kumuelimisha msichana ni kuijenga familia, jamii na taifa. Elimu ni injini ya mageuzi ya kijamii,” amesema. Ameeleza kuwa elimu inapaswa kuwa ya vitendo na inayomuandaa kijana kuishi kwa heshima, kutatua changamoto za maisha pamoja na kuchangia maendeleo ya jamii. Aidha, amepongeza juhudi zinazofanywa na taasisi mbalimbali katika kuhamasisha elimu ya kujiamini na ubunifu. Dkt. Kamm, kupitia Taasisi ya Mama Clementina, amekuwa mstari wa mbele katika ujenzi wa miundombinu ya shule, kuwezesha watoto wa kike kupata fursa za masomo na kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika sekta ya elimu. Kwa upande mwingine, amewataka wahitimu kutokata tamaa wanapokutana na vikwazo katika safari yao ya kutafuta mafanikio. “Elimu yenu ndiyo nguvu yenu. Itumieni kwa uadilifu na malengo makubwa, na msisahau mizizi yenu,” amesisitiza. Katika hotuba yake, Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. William Anangisye, amesema UDSM imepitia jumla ya mitaala zaidi ya 250, ambapo mitaala 242 ya Shahada ya Awali na Uzamili tayari imewasilishwa TCU kwa ajili ya uthibitisho. “Hadi sasa mitaala 49 imepata ithibati kwa mwaka wa masomo 2025/2026,” amesema. Ameongeza kuwa chuo kimewezesha kutambuliwa kwa bunifu zaidi ya 120 na kusajili kampuni changa 39 ambazo ni zao la ubunifu wa wanafunzi na wahadhiri, ikiwa ni sehemu ya kukuza ujasiriamali nchini. Kuhusu mafunzo ya ubunifu na ujasiriamali, Prof. Anangisye amesema UDSM imetoa mafunzo hayo kwa wanafunzi 569, wakiwemo wanafunzi 65 wenye ulemavu, jambo ambalo linadhihirisha dhamira ya chuo kujenga mazingira jumuishi kwa maendeleo endelevu. Jumla ya wahitimu 2,742 walihudhurishwa kwenye mahafali hayo yaliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam. Kati ya wahitimu hao, wanawake ni 1,510 sawa na asilimia 55.0, huku wanaume wakiwa 1,232. Gen Z watupu! Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

MATAIFA 8 KUIMBA TAMASHA LA PASAKA

PIMEA USIKU WA WANA NDOA ULIVYOFANA MSIFICHANE NA KUWEKEANA VITU

UONGOZI DHAIFU VYATAJWA KUVURUGA TAASISI ZA VIJANA