WASANII WATAKIWA MAONI
Serikali kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo imewataka wasanii kushiriki kikamilifu katika utoaji wa maoni ya maboresho ya itifaki ya Beijing ya 2012 kwa kuwa ni mpango uliolenga kuwanufaisha.
Hayo yamesemwa Dar es Salaam na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa wa Wizara hiyo Venance Mwamengo wakati akifungua mkutano wa wadau wa ubunifu kujadili itifaki hiyo, ulioandaliwa na Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (Cosota) kwa kushirikiana na Shirika la Miliki Bunifu la kikanda la Afrika (ARIPO).
Amesema ushiriki wao kwa pamoja ni kuunga mkono juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan ambaye anataaka kuona maamuzi shirikishi.
"Serikali ina wajibu wa kuhakikisha kuwa wasanii na wabunifu wanalindwa na sheria na wananufaika ndio maana imeweka mazingira rafiki ili kuhakikisha wasanii, waandishi na wabunifu wananufaika na Sheria ya Hakimiliki na haki bunifu kwa hivyo ni muhimu washiriki kutoa maoni,"amesema.
Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Cosota Doreen Sinare amesema wadau wote wa ubunifu wakiridhia itifaki hiyo itabadilishwa kuendana na Sheria.
"Cosota kupitia Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo pamoja na wizara nyingine tumeamua tuweke nguvu kuhakikisha itifaki zote zinazohusiana na miliki bunifu tunaziridhia kama nchi ili nchi iweze kunufaika zaidi,"amesema na kuongeza kuwa mwezi ujao watakutana kwenye mkutano mkubwa wa wadau na itifaki zote muhimu zitapelekwa kwa wadau ili nchi iweze kiziridhia.
Amesema mpango huo utawanufaisha wasanii, waigizaji,waandaaji, watayarishaji na kuweza kupata kipato kutokana na matumizi ya kazi zao kwenye mitandao.


Comments
Post a Comment